Monday 5 March 2018

Katibu Mkuu wa Nishati akutana na Kampuni ya Rift Valley Energy

Na Zuena msuya Dodoma.

Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. Hamis Mwinyimvua amekutana na Kampuni ya Rift Valley Energy inayotaka kuzalisha umeme kwa kutumia nguvu ya upepo Mkoani Njombe.

Dkt.Mwinyimvua amekutana na Kampuni hiyo katika Makao Makuu ya Wizara ya Nishati Mkoani Dodoma.



Katika mazungumzo hayo Kampuni hiyo imesema kuwa mbali na kutaka kuzalisha Umeme wa upepo, tayari kampuni hiyo inazalisha umeme wa Megawati 4 kwa kutumia maporomoko ya maji katika eneo Mwenga mkoani Njombe na kuusambaza kwenye vijiji 34 vinavyozunguka eneo hilo.

Aidha kampuni hiyo pia itatekeleza miradi mingine ya umeme kwa kutumia maporomoko madogo ya katika maeneo ya Luponda Mkoani Njombe na Suma Mkoani Mbeya.




Wakazi wa DSM kuanza kutumia gesi asilia kwa matumizi ya Nyumbani

Na Zuena Msuya Dodoma,

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amelitaka na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuharakisha uunganishaji wa huduma ya gesi asilia katika baadhi ya nyumba za wananchi kwenye maeneo ya jiji la Dar Es Salaam kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.

Dkt.Kalemani aliyasema hayo ofisini kwake mkoani Dodoma alipokutana na watendaji wa TPDC kwa lengo la kujadili suala la usambazaji wa Gesi asilia katika nyumba za Wananchi pamoja na bei watakayouziwa wananchi hao.

Katika mazungumzo hayo, Dkt. Kalemani aliwataka TPDC kuunganisha  nyumba  kuanzia Hamsini( 50) na kuendelea, na huduma ya gesi asilia katika  maeneo la Mwenge na Mikocheni, kwa kuwa tayari miundombinu ya bomba la gesi asilia kwa matumizi ya nyumbani imepita maeneo hayo.

Wakizungumzia suala la bei ya kuwauzia wateja, Dkt. Kalemani alisema kuwa pamoja na mambo mengine Gesi hiyo itauzwa kwa Wananchi kwa pungufu ya 40% ya bei ya mitungi ya gesi itayokuwa sokoni kwa wakati huo.

" Hii ni gesi yetu na bomba ni la kwetu vyote vinapatikana hapahapa nchini, ni vyema iuzwe kwa bei ya chini zaidi ya ile iliyopo sokoni kwa sasa, ili kila mwananchi aweze kumudu gharama zake pia ni rafiki wa mazingira, itasaidia kupunguza matumizi ya mkaa na kulinda misitu yetu", alisema Dkt. Kalemani.

Hata Hivyo Dkt. Kalemani aliwaagiza TPDC kuendelea na taratibu za kuwaunganisha wananchi wa Mtwara na huduma ya gesi asilia katika nyumba zao kwa matumizi ya nyumbani kama itavyofanyika jijini Dar es salaam hivi karibuni.

Aidha amelishauri shirika hilo, kutumia wataalamu wake wa ndani kupitia shirika lake la kulinda miundombinu ya gesi (GASCO) ili kusambaza gesi asilia kwenye nyumba za wananchi kwa ajili ya matumizi ya nyumbani badala ya kutegemea wakandarasi ambao mchakato wa kuwapata unachukuwa muda mrefu.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa TPDC, Mhandisi Kapuulya Musomba, alifafanua kuwa gharama za uunganishwaji wa huduma ya gesi asilia katika nyumba za wananchi itategemea na ramani ya nyumba husika pamoja na umbali wa nyumba hiyo kutoka ilipopita miundombinu ya bomba la gesi asilia linalotumika kusambaza gesi katika maeneo ya makazi.

Vilevile, Mhandisi Musomba aliweka wazi kuwa mfumo wa kusambaza gesi asilia katika nyumba za wananchi utakuwa kama ule unaotumika kusambaza huduma ya maji, lakini ulipaji wa gharama za matumizi ya gesi hiyo utakuwa kama ule unaotumiwa na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Lipa Umeme Kadri Unavyotumia (LUKU) kwa maana kwamba kila mtumiaji wa gesi asilia nyumbani kwake atalipia huduma hiyo kwa kadri atakavyokuwa akitumia.

Gesi itakayokuwa ikisambazwa kwa ajili ya matumizi ya nyumbani ni ile inayozalishwa katika Visima vya gesi vilivyopo katika Mkoa wa Lindi na Mtwara. 


Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani akizungumza na watendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) na watendaji wa Wizara ya Nishati, kuhusua suala la usambazaji wa gesi asilia katika nyumba za wananchi kwa ajili ya matumizi ya nyumbani, ofisini kwake mkoani Dodoma

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (kushoto) na Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Mhandisi Kapuulya Msomba (kulia) wakizungumza kuhus suala la usambazaji wa gesi asilia katika nyumba za wananchi kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.

Hatua za kisheria kuchukuliwa kwa Wakandarasi watakaoshindwa kuunganisha Umeme katika Vijiji Vitatu (3) ndani ya siku 7

Na. Zuena Msuya, Simiyu

Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani amewaagiza wakuu wa wilaya kote nchini kuwachukulia hatua za kisheria wakandarasi watakaoshindwa kuunganisha vijiji kuanzia vitatu (3) na kuendelea wakati wakitekeleza mradi wa usambazaji wa umeme vijijini Awamu ya Tatu (REA III). 

Dkt. Medard Kalemani aliyasema hayo wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua maendeleo ya utekelezaji wa mradi wa REA III katika vijiji vya Gumali na Malampaka vilivyopo wilayani Maswa mkoani Simiyu.

Aliweka wazi kuwa wakandarasi wote waliokwisha anza utekelezaji wa REA III wanatakiwa kuunganisha vijiji kuanzia vitatu (3) na kuendelea ili kuwatia hamasa wananchi katika kujiunga na huduma ya umeme.

Alisema zoezi hilo litaongeza chachu kwa wananchi kuanzisha viwanda vidogo vidogo na hata vikubwa mapema zaidi ili kuunga mkono azma ya Serikali ya Awamu ya Tano katika kutimiza sera yake ya kuwa na viwanda nchini kote.

"Kila mkandarasi aliyekwishaanza kazi ya kutekeleza Mradi wa REA III, anatakiwa kuunganisha huduma ya umeme katika vijiji 3 na kuendelea ndani ya wiki moja, haya ni makubaliano, atakayeshindwa kufanya hivyo, Mkuu wa Wilaya husika atamkamata na kumtia ndani ", alisistiza Dkt. Kalemani.

Vilevile aliwaagiza Wakuu hao wa wilaya  kwa kushirikiana na Mameneja wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa Mradi wa REA III katika maeneo yao ili kuweza kufikia lengo lililokusudiwa la kuunganisha vijiji vyote na vitongoji vyake ifikapo mwaka 2021.

Aliwasisitiza wakandarasi kuwa ili kurahisisha utendaji kazi wao na kupunguza gharama watumie  nguvu kazi kutoka katika maeneo yanayozunguka  mradi husika ili wananchi wa maeneo hayo waweze kunufaika na mradi huo kwa namna moja au nyingine na si kuchukua wafanyakazi kutoka mbali na eneo la mradi.

Akizungumzia hali ya upatikanaji wa umeme katika mkoa wa Simiyu, Dkt. Kalemani alisema ifikapo mwezi Mei mwaka huu wataanza kujenga vituo viwili vya kupokea na kupoza umeme ili kupunguza adha ya kukatika mara kwa mara kwa huduma ya umeme katika mkoa huo. Adha ya kukatika kwa umeme unatokana na umeme kusafirishwa umbali mrefu kutoka Mkoa wa Mwanza na Mara.

Kwa upande wake, Mbunge wa Maswa Magharibi,  Mashimba Ndaki aliwasihi wananchi katika vijiji vyote vinavyopitiwa na mradi wa REA III  kuchangamkia fursa ya kuunganishwa na huduma ya umeme wa REA III kwa kuwa ni wa bei nafuu ya shilingi elfu Ishirini na Saba tu (27,000).

Hata hivyo aliwataka wale wote ambao bado hawajafanya wiring katika nyumba zao kufanya hivyo haraka. Aidha, kwa wale wenye nyumba za nyasi wawe tayari kutumia kifaa kinachoitwa Umeme Tayari (UMETA) wakati wa utekelezaji wa mradi huo.

Pia amewaomba wakandarasi wanaotekeleza miradi ya REA III kushirikiana na Serikali za vijiji na Mitaa wanapokuwa wakihitaji nguvu kazi ya vijana ili waweze kupata vijana waaminifu na wenye kufanya kazi kwa uzalendo. 

Waziri wa Nishati Dkt. Kalemani (katikati) akizungumza na wakazi wa kijiji cha Gumali, wilayani Maswa alipofika kukagua mradi wa REA III.

Waziri wa Nishati Dkt. Kalemani (katikati), mbunge wa Maswa Magharibi, Mashimba Ndaki( kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Maswa( kulia) Dkt. Seif Shekalaghe wakikagua orodha ya vijiji vitakavyopitiwa na Mradi wa REA III katika mzunguko wa kwanza wa REA IIII.


 
Waziri wa Nishati Dkt. Medard  Kalemani (kulia), na Kaimu Kamishna wa Nishati na Maendeleo ya Petroli,  Mhandisi Innocent Luoga wakikagua Miundombinu ya umeme iliyoanguka kutokana na upepo mkali uliombatana na mvua wilayani Maswa na kusababisha baadhi ya vijiji kukosa huduma ya umeme kwa siku kadhaa.


Kikundi cha ngoma ya asili kikitumbuiza kufurahia huduma ya umeme kufika katika kijiji cha Gumali wilayani Maswa, mkoani Simiyu.