Monday 5 March 2018

Wakazi wa DSM kuanza kutumia gesi asilia kwa matumizi ya Nyumbani

Na Zuena Msuya Dodoma,

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amelitaka na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuharakisha uunganishaji wa huduma ya gesi asilia katika baadhi ya nyumba za wananchi kwenye maeneo ya jiji la Dar Es Salaam kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.

Dkt.Kalemani aliyasema hayo ofisini kwake mkoani Dodoma alipokutana na watendaji wa TPDC kwa lengo la kujadili suala la usambazaji wa Gesi asilia katika nyumba za Wananchi pamoja na bei watakayouziwa wananchi hao.

Katika mazungumzo hayo, Dkt. Kalemani aliwataka TPDC kuunganisha  nyumba  kuanzia Hamsini( 50) na kuendelea, na huduma ya gesi asilia katika  maeneo la Mwenge na Mikocheni, kwa kuwa tayari miundombinu ya bomba la gesi asilia kwa matumizi ya nyumbani imepita maeneo hayo.

Wakizungumzia suala la bei ya kuwauzia wateja, Dkt. Kalemani alisema kuwa pamoja na mambo mengine Gesi hiyo itauzwa kwa Wananchi kwa pungufu ya 40% ya bei ya mitungi ya gesi itayokuwa sokoni kwa wakati huo.

" Hii ni gesi yetu na bomba ni la kwetu vyote vinapatikana hapahapa nchini, ni vyema iuzwe kwa bei ya chini zaidi ya ile iliyopo sokoni kwa sasa, ili kila mwananchi aweze kumudu gharama zake pia ni rafiki wa mazingira, itasaidia kupunguza matumizi ya mkaa na kulinda misitu yetu", alisema Dkt. Kalemani.

Hata Hivyo Dkt. Kalemani aliwaagiza TPDC kuendelea na taratibu za kuwaunganisha wananchi wa Mtwara na huduma ya gesi asilia katika nyumba zao kwa matumizi ya nyumbani kama itavyofanyika jijini Dar es salaam hivi karibuni.

Aidha amelishauri shirika hilo, kutumia wataalamu wake wa ndani kupitia shirika lake la kulinda miundombinu ya gesi (GASCO) ili kusambaza gesi asilia kwenye nyumba za wananchi kwa ajili ya matumizi ya nyumbani badala ya kutegemea wakandarasi ambao mchakato wa kuwapata unachukuwa muda mrefu.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa TPDC, Mhandisi Kapuulya Musomba, alifafanua kuwa gharama za uunganishwaji wa huduma ya gesi asilia katika nyumba za wananchi itategemea na ramani ya nyumba husika pamoja na umbali wa nyumba hiyo kutoka ilipopita miundombinu ya bomba la gesi asilia linalotumika kusambaza gesi katika maeneo ya makazi.

Vilevile, Mhandisi Musomba aliweka wazi kuwa mfumo wa kusambaza gesi asilia katika nyumba za wananchi utakuwa kama ule unaotumika kusambaza huduma ya maji, lakini ulipaji wa gharama za matumizi ya gesi hiyo utakuwa kama ule unaotumiwa na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Lipa Umeme Kadri Unavyotumia (LUKU) kwa maana kwamba kila mtumiaji wa gesi asilia nyumbani kwake atalipia huduma hiyo kwa kadri atakavyokuwa akitumia.

Gesi itakayokuwa ikisambazwa kwa ajili ya matumizi ya nyumbani ni ile inayozalishwa katika Visima vya gesi vilivyopo katika Mkoa wa Lindi na Mtwara. 


Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani akizungumza na watendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) na watendaji wa Wizara ya Nishati, kuhusua suala la usambazaji wa gesi asilia katika nyumba za wananchi kwa ajili ya matumizi ya nyumbani, ofisini kwake mkoani Dodoma

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (kushoto) na Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Mhandisi Kapuulya Msomba (kulia) wakizungumza kuhus suala la usambazaji wa gesi asilia katika nyumba za wananchi kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.