Na
Greyson Mwase, Dar es Salaam
Leo tarehe 10 Aprili,
2018, Kamishna wa Nishati, Mhandisi Innocent Luoga amefanya ziara katika kampuni
ya Mantrac iliyopo jijini Dar es Salaam ambapo aliambatana na wataalam kutoka
Wizara ya Nishati na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO). Lengo la ziara yake
lilikuwa ni kukagua maendeleo ya mitambo miwili ya kuzalisha umeme kwa kutumia
gesi iliyoingizwa nchini na kampuni ya Mantrac kwa ajili ya kusimikwa kwenye
kituo cha kuzalisha umeme kwa kutumia gesi cha Mtwara ambapo kila mtambo una
uwezo wa Megawati 2.
Akielezea hatua iliyofikiwa ya uingizwaji wa mitambo na
vifaa vyake kwa Kamishna Luoga, Meneja Miradi kutoka kampuni ya Mantrac, Ahmed
Maamoun alisema kazi inayoendelea kwa sasa ni uundwaji wa mitambo pamoja
na vifaa vyake kabla ya kusafirishwa
katika kituo za kuzalisha umeme cha Mtwara kwa ajili ya usimikwaji.
Maamoun aliongeza kuwa
msingi kwa ajili ya usimikaji wa mitambo husika umekamilika na kusisitiza kuwa
Mantrac inafanya kazi usiku na mchana katika kuhakikisha kuwa mradi unakamilika
mapema na kukabidhiwa kwa serikali
Naye Kamishna Luoga
alisema kuwa, Serikali ipo tayari kushirikiana na kampuni ya Mantrac ili mradi
uweze kukamilika kwa wakati na kusisitiza kuwa wananchi wa Mtwara wanahitaji
umeme kwa ajili ya shughuli zao za kiuchumi.
Meneja Miradi kutoka
kampuni ya Mantrac, Ahmed Maamoun (kulia) akielezea majukumu ya kampuni kwa
Kamishna wa Nishati, Mhandisi Innocent Luoga (kushoto) katika ziara hiyo.
|
Alisema kuwa mahitaji
ya umeme katika mkoa wa Mtwara yanazidi kuongezeka na kufafanua kuwa Serikali
kupitia Wizara ya Nishati imeweka mikakati ya muda mfupi na mrefu katika
kuhakikisha kuwa nishati ya uhakika na ya gharama nafuu inapatikana.
Aliendelea kusema ununuzi wa mitambo husika ni moja ya
mikakati ya muda mfupi ya Wizara ya Nishati katika kutatua changamoto
ya upatikanaji wa umeme wa kutosha
katika mkoa wa Mtwara.
Alitaja mikakati ya
muda mrefu kuwa ni pamoja na ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme kwa kutumia
gesi asilia chenye uwezo wa kuzalisha Megawati 300 mkoani Mtwara na kituo
kingine cha Somangafungu chenye uwezo wa Megawati 330 mkoani Lindi.
Katika hatua nyingine
Mhandisi Luoga mbali na kupongeza kampuni ya Mantrac katika utekelezaji wa
mradi husika, aliitaka kampuni kuongeza
kasi ili kuhakikisha mradi unakamilika na kukabidhiwa kwa Serikali kabla
ya mwisho wa mwezi Aprili.
“Mradi huu ni muhimu
sana kwa kuwa tunahitaji wananchi wa Mtwara wapate umeme wa uhakika ndani ya
kipindi cha muda mfupi, kasi inahitajika na pale mtakapokwama katika
utekelezaji wa mradi msisite kuwasiliana na Serikali ili iweze kuwasaidia,” alisisitiza Mhandisi
Luoga.
Meneja Miradi kutoka
kampuni ya Mantrac, Ahmed Maamoun akifafanua jambo kwa Kamishna wa Nishati,
Mhandisi Innocent Luoga (kushoto) katika ziara hiyo.
|