- Waziri Kalemani asema wanakaribishwa ikiwa wana vigezo
Na
Veronica Simba – Dodoma
Wawekezaji kutoka
Kampuni ya Hainan Zhenrong Energy Ltd ya China wamemtembelea Waziri wa Nishati
Dkt. Medard Kalemani na kumweleza nia yao ya kuwekeza katika sekta ya nishati
nchini; hususan kwenye sekta ndogo ya gesi asilia.
Ujumbe huo kutoka China
ukiongozwa na Mwenyekiti wa Kampuni hiyo, Li Zemng, waliwasilisha maombi husika
kwa Waziri na timu yake ya wataalam kutoka wizarani na TANESCO, Aprili 11, 2018
Makao Makuu ya Wizara mjini Dodoma.
Zemng alimweleza Waziri
Kalemani kuwa nia yao ni kuwezesha usafirishaji wa gesi asilia katika maeneo
mbalimbali nchini ambako bomba la gesi halifiki kwa kutumia teknolojia maalum.
“Tutatumia teknolojia
maalum kuigeuza gesi asilia katika hali ya kimiminika (Liquefied Natural Gas –
LNG), kisha tutaihifadhi katika makontena maalum na kuyasafirisha kwenda maeneo
mbalimbali ambako itatumika kwa shughuli mbalimbali za maendeleo,” alifafanua Zemng.
Akijibu maombi hayo,
Waziri Kalemani alisema Serikali inakaribisha wawekezaji katika sekta husika
lakini akatahadharisha kuwa ni lazima wawe na vigezo stahiki.
Alitoa mwongozo kwa
Kampuni hiyo kuwasilisha maombi yao rasmi kimaandishi ili yafanyiwe kazi.
Aidha, aliwataka kukutana na timu ya wataalam kutoka wizarani na TANESCO ili
wajadiliane kwa kina kuhusu maombi hayo ya uwekezaji ili kujiridhisha kabla ya
kuwapatia jibu rasmi.