- Waunganishwa kwenye Gridi ya Taifa
Na
Veronica Simba - Ngara
Wilaya ya Ngara mkoani
Kagera imeunganishwa kwenye umeme wa Gridi ya Taifa na kuachana na matumizi ya
umeme wa mafuta ya dizeli.
Hafla ya ufunguzi wa
matumizi ya umeme wa Gridi ya Taifa wilayani humo ilifanyika Aprili 8 mwaka huu
na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, Vyama vya Siasa, Dini na
wananchi ambapo Mgeni Rasmi alikuwa Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani.
Meneja wa TANESCO Mkoa
wa Kagera, Mhandisi Francis Maze, akielezea mawanda ya Mradi huo alisema
umehusisha kujenga njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33, yenye urefu wa
kilomita 42 kutoka Nyakahura wilayani Biharamulo hadi Benaco wilayani Ngara.
Vilevile, alisema Mradi
umejumuisha kazi ya kujenga njia za umeme za michepuko za msongo wa kilovoti 33
zenye jumla ya urefu wa kilomita 27.5 ili kulisha umeme katika vijiji vya
Kabulwanzwiri, Kabaheshi, Lukore, Kibilizi na Keza Sekondari.
“Hii inafanya jumla ya
urefu wa njia za umeme za msongo wa kilovoti 33 zinazojengwa kuwa kilomita
69.5,” alifafanua Mhandisi Maze.
Aidha, alitaja kazi
nyingine kuwa ni kujenga na kuweka mashine umba (Transfoma) 10 kwa vijiji na
vitongoji vilivyohusishwa na Mradi.
Nyingine ni ujenzi wa
njia za msongo mdogo wa umeme zenye jumla ya kilomita 19 katika vijiji 10
vilivyonufaika na Mradi.
Kuhusu idadi ya wateja
watakaonufaika na Mradi huo, Mhandisi Maze alisema kuwa jumla yao ni 482 kutoka
katika vijiji vya Nyantama (53), Nyabugombe (74), Lukole (51), Kabaheshi (101)
na Kabulwanzwiri (58).
Vijiji vingine ni
Kumyaga (20), Mtega (68), Gwishushi (17), Kibilizi (30) na Keza (10).
Manufaa makubwa ambayo
Mhandisi Maze alisema TANESCO itayapata kutokana na Mradi huo wa kuiunga Ngara
kwenye umeme wa Gridi ya Taifa ni kupungua kwa gharama za uendeshaji ambapo
sasa shirika hilo litapata nafuu ya asilimia 73.4 katika gharama za kupata
Uniti moja ya umeme. Aidha, wananchi watapata umeme wa uhakika zaidi.
Hata hivyo, Meneja huyo
wa Mkoa wa Kagera alitaja changamoto kubwa ambazo Ofisi yake inakabiliana nazo
kuwa ni uchakavu wa miundombinu ya usambazaji umeme, hususan njia za umeme za
Msongo wa kilovoti 33 za Muleba, Kanyigo na Karagwe.
Alitaja changamoto
nyingine kuwa ni wananchi kuzuia kukatwa kwa matawi ya miti yanayosonga njia za
umeme mkubwa na kuipeleka TANESCO Mahakamani pale inapolazimu kukatwa kwa miti
hiyo.
Nyingine ni wananchi
kupanda miti ya mbao jirani mno na njia za umeme na kusababisha miti hiyo
kugusa nyaya kukiwa na upepo mkali hivyo kusababisha kukatika kwa umeme.
Changamoto nyingine
iliyotajwa kuikabili TANESCO mkoani Kagera kuwa ni wananchi kuchoma nguzo za
umeme, hususan za njia za umeme zilizopita mashambani.
Aliwataka wananchi
kutoa ushirikiano kwa Shirika hilo ili kuepusha na kutatua changamoto hizo,
hali itakayosaidia kuboresha zaidi huduma zao na hivyo jamii kunufaika zaidi.
Sehemu ya viongozi
mbalimbali wa serikali na vyama vya siasa wakiwa katika hafla ya ufunguzi wa
matumizi ya umeme wa Gridi ya Taifa wilayani Ngara, Aprili 8 mwaka huu.
|