Saturday 14 April 2018

Serikali yapongeza utendaji wa Tanesco

Na Veronica Simba - Ngara

Serikali imelipongeza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kutokana na utendaji kazi wake mzuri katika kuwapatia watanzania kote nchini huduma ya nishati ya umeme.
 
Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa matumizi ya umeme wa Gridi ya Taifa wilayani Ngara, Aprili 8 mwaka huu.
Pongezi hizo zilitolewa hivi karibuni, Aprili 8 mwaka huu, na Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani wakati wa hafla ya ufunguzi wa matumizi ya umeme wa Gridi ya Taifa wilayani Ngara.

“Nalipongeza Shirika letu la TANESCO. Kwakweli Shirika hili limebadilika sana kiutendaji, hasa katika Menejimenti na wafanyakazi. Wanafanya kazi kwa kujituma. Baadhi ya watu walizoea kulibeza Shirika hili lakini wanajitahidi sana kwa sasa,” alisema Waziri.
Waziri alisema kuwa kazi ya Serikali kupitia Wizara ya Nishati ni kulisimamia Shirika hilo ili liendelee kufanya kazi nzuri kwa manufaa ya wananchi.
Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Dkt. Tito Mwinuka akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa matumizi ya umeme wa Gridi ya Taifa wilayani Ngara, Aprili 8 mwaka huu.

 Akizungumzia Mradi huo wa kuiunganisha Ngara na umeme wa Gridi ya Taifa, Waziri Kalemani alisema kuwa ni wa manufaa makubwa kwani utapunguza kwa kiasi kikubwa gharama za uendeshaji na hivyo kuliongezea shirika uwezo zaidi wa kuwahudumia wananchi.
“Kwa kutumia mafuta, Uniti moja ilikuwa inawagharimu TANESCO shilingi 578 wakati huu wa Gridi utawagharimu shilingi 154 tu kwa Uniti,” alifafanua.

Waziri aliwataka watendaji wa TANESCO kuhakikisha wanawahudumia wana-Ngara na watanzania wote kwa ubora zaidi kutokana na uwepo wa umeme wa Gridi ya Taifa katika maeneo mengi zaidi na kuondokana na ule wa mafuta ambao una changamoto kadhaa.

Aidha, Dkt. Kalemani alibainisha kuwa, sambamba na zoezi la kuhakikisha Tanzania nzima inaunganishwa na umeme wa Gridi ya Taifa, pia Serikali inaendelea kupeleka umeme vijijini kupitia miradi inayotekelezwa kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
Alisema kuwa, kufikia mwaka 2020, hakuna kijiji kitakachobaki bila kuwa na umeme.
Meneja wa TANESCO Mkoa wa Kagera, Mhandisi Francis Maze akiwasilisha taarifa ya Mkoa wake kwa Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani, wakati wa hafla ya ufunguzi wa matumizi ya umeme wa Gridi ya Taifa wilayani Ngara, Aprili 8 mwaka huu.

Aliipongeza Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais John Magufuli kwa dhamira yake ya dhati katika kuhakikisha inawaondolea watanzania kero na changamoto mbalimbali ikiwemo ya umeme.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Dkt. Tito Mwinuka pamoja na kumuunga mkono Waziri kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano; aliipongeza Wizara ya Nishati inayoongozwa na Dkt Kalemani ambayo alisema ndiyo msimamizi mkubwa wa shughuli zinazotekelezwa na shirika hilo.

Alisema kuwa, kwa kuiunga Ngara na umeme wa Gridi ya Taifa, kiasi kikubwa cha fedha kitaokolewa. “Kwa harakaharaka, tutaweza kuokoa takribani shilingi bilioni mbili kwa mwaka baada ya kuzima mitambo hii ya mafuta.”

Aliongeza kusema kuwa TANESCO itaendelea kuzima vituo vya mafuta sehemu mbalimbali nchini ambapo itasaidia kupunguza gharama za kufua umeme kwa kutumia mafuta.


Awali, akiwasilisha taarifa ya TANESCO kwa Mkoa wa Kagera, Meneja wake, Mhandisi Francis Maze alisema kuwa kabla ya kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa, Wilaya ya Ngara ilikuwa ikitumia umeme wa mafuta ambapo mahitaji ya juu kwa Wilaya hiyo ni megawati 1.38.
Kaimu Meneja Uhusiano wa TANESCO, Leyla Muhaji akifurahia ngoma pamoja na kikundi cha burudani kilichokuwa kikitumbuiza wakati wa hafla ya ufunguzi wa matumizi ya umeme wa Gridi ya Taifa wilayani Ngara, Aprili 8 mwaka huu.