Na
Veronica Simba – Dodoma
Waziri wa Nishati Dkt.
Medard Kalemani ameshiriki majadiliano ya maendeleo ya miradi mbalimbali ya
Serikali inayofadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).
Majadiliano hayo yalifanyika
Aprili 11 mwaka huu Ofisi za Wizara ya Fedha na Mipango Dodoma na kuwashirikisha
Waziri husika, Dkt. Philip Mpango, Waziri Kalemani, mwakilishi kutoka Wizara ya
Fedha ya Zanzibar, Halima Wagao, wataalam mbalimbali wa Wizara hizo na Ujumbe
kutoka AfDB.
Akizungumza katika
kikao hicho, Waziri Kalemani aliipongeza na kuishukuru Benki hiyo kwa
ushirikiano ambao imekuwa ikiuonesha, hususan katika kufadhili miradi
mbalimbali ya maendeleo kwa sekta ya nishati.
Miradi ya nishati iliyojadiliwa
katika kikao husika ni pamoja na wa Malagarasi unaohusisha kuzalisha umeme wa
megawati 45 pamoja na mradi wa kuzalisha umeme wa Kakono wenye megawati 87.
Aidha, miradi mingine
ni pamoja na wa kusafirisha umeme wa kilovoti 220 kutoka Rusumo hadi Nyakanazi
na wa kusafirisha umeme wa kilovoti 400 kutoka Singida – Arusha hadi Namanga.
Vilevile, mradi wa kusafirisha umeme wa kilovoti 400 kwa umbali wa kilomita 280
kutoka Nyakanazi hadi Kigoma.
Kwa mujibu wa Afisa
Nishati Mkuu kutoka Wizara ya Nishati, Mhandisi Salum Inegeja, miradi yote hiyo
inafadhiliwa na AfDB kwa namna mbili ambazo ni ama kwa ufadhili wa asilimia
kadhaa kwa kushirikiana na wadau wengine au ufadhili wa asilimia 100.
Kuhusu hatua ambazo
Serikali imechukua katika kuhakikisha inaboresha utendaji wa TANESCO; suala
ambalo Ujumbe wa AfDB ulitaka kujuzwa; Waziri Kalemani alisema uboreshaji huo
unahitaji kupitia hatua kadhaa ambazo tayari Serikali imeshaanza kuzitekeleza.
Alizitaja hatua hizo
kuwa ni pamoja na kupiga marufuku uagizaji kutoka nje ya nchi, vifaa mbalimbali
kama vile nguzo, mashine-umba (transfoma), waya na mita za umeme na badala yake
vinunuliwe kwa wazalishaji wa ndani ya nchi.
Alieleza hatua nyingine
iliyochukuliwa na Serikali kuwa ni kufupisha muda wa kuwaunganishia wateja huduma
ya umeme. “Wateja sasa wanaunganishwa ndani ya siku zisizozidi Saba tofauti na
awali ambapo zoezi hilo lilikuwa likichukua muda mrefu zaidi.”
Vilevile, Waziri
alieleza kuwa Serikali inazungumza na kampuni za ugavi na usambazaji ambazo
zinaidai TANESCO madeni makubwa kusamehe tozo za riba kwa shirika hilo ili
kulipunguzia mzigo.
Aidha, hatua nyingine
iliyochukuliwa ni kuanzisha na kuwafungia wateja wote mfumo wa Mita za umeme za
LUKU zinazowezesha kufanyika kwa malipo ya umeme kadri ya matumizi ya mteja
husika.
Mawaziri Kalemani na
Mpango, waliahidi kuwa Serikali itaweka jitihada za makusudi katika kuhakikisha
kwa upande wao wanatekeleza kwa wakati majukumu yote waliyoafikiana ili
kuwezesha miradi yote inayohusika inatekelezwa kikamilifu na kwa wakati kama
ilivyopangwa kwa manufaa ya wananchi na Taifa kwa ujumla.
Waliwaagiza wataalam
katika Wizara zao kukutana na kujadiliana na wataalam kutoka AfDB ili kuweka
mambo sawa, kwa ajili ya kuharakisha utekelezaji wa miradi husika.