Monday 5 March 2018

Hatua za kisheria kuchukuliwa kwa Wakandarasi watakaoshindwa kuunganisha Umeme katika Vijiji Vitatu (3) ndani ya siku 7

Na. Zuena Msuya, Simiyu

Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani amewaagiza wakuu wa wilaya kote nchini kuwachukulia hatua za kisheria wakandarasi watakaoshindwa kuunganisha vijiji kuanzia vitatu (3) na kuendelea wakati wakitekeleza mradi wa usambazaji wa umeme vijijini Awamu ya Tatu (REA III). 

Dkt. Medard Kalemani aliyasema hayo wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua maendeleo ya utekelezaji wa mradi wa REA III katika vijiji vya Gumali na Malampaka vilivyopo wilayani Maswa mkoani Simiyu.

Aliweka wazi kuwa wakandarasi wote waliokwisha anza utekelezaji wa REA III wanatakiwa kuunganisha vijiji kuanzia vitatu (3) na kuendelea ili kuwatia hamasa wananchi katika kujiunga na huduma ya umeme.

Alisema zoezi hilo litaongeza chachu kwa wananchi kuanzisha viwanda vidogo vidogo na hata vikubwa mapema zaidi ili kuunga mkono azma ya Serikali ya Awamu ya Tano katika kutimiza sera yake ya kuwa na viwanda nchini kote.

"Kila mkandarasi aliyekwishaanza kazi ya kutekeleza Mradi wa REA III, anatakiwa kuunganisha huduma ya umeme katika vijiji 3 na kuendelea ndani ya wiki moja, haya ni makubaliano, atakayeshindwa kufanya hivyo, Mkuu wa Wilaya husika atamkamata na kumtia ndani ", alisistiza Dkt. Kalemani.

Vilevile aliwaagiza Wakuu hao wa wilaya  kwa kushirikiana na Mameneja wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa Mradi wa REA III katika maeneo yao ili kuweza kufikia lengo lililokusudiwa la kuunganisha vijiji vyote na vitongoji vyake ifikapo mwaka 2021.

Aliwasisitiza wakandarasi kuwa ili kurahisisha utendaji kazi wao na kupunguza gharama watumie  nguvu kazi kutoka katika maeneo yanayozunguka  mradi husika ili wananchi wa maeneo hayo waweze kunufaika na mradi huo kwa namna moja au nyingine na si kuchukua wafanyakazi kutoka mbali na eneo la mradi.

Akizungumzia hali ya upatikanaji wa umeme katika mkoa wa Simiyu, Dkt. Kalemani alisema ifikapo mwezi Mei mwaka huu wataanza kujenga vituo viwili vya kupokea na kupoza umeme ili kupunguza adha ya kukatika mara kwa mara kwa huduma ya umeme katika mkoa huo. Adha ya kukatika kwa umeme unatokana na umeme kusafirishwa umbali mrefu kutoka Mkoa wa Mwanza na Mara.

Kwa upande wake, Mbunge wa Maswa Magharibi,  Mashimba Ndaki aliwasihi wananchi katika vijiji vyote vinavyopitiwa na mradi wa REA III  kuchangamkia fursa ya kuunganishwa na huduma ya umeme wa REA III kwa kuwa ni wa bei nafuu ya shilingi elfu Ishirini na Saba tu (27,000).

Hata hivyo aliwataka wale wote ambao bado hawajafanya wiring katika nyumba zao kufanya hivyo haraka. Aidha, kwa wale wenye nyumba za nyasi wawe tayari kutumia kifaa kinachoitwa Umeme Tayari (UMETA) wakati wa utekelezaji wa mradi huo.

Pia amewaomba wakandarasi wanaotekeleza miradi ya REA III kushirikiana na Serikali za vijiji na Mitaa wanapokuwa wakihitaji nguvu kazi ya vijana ili waweze kupata vijana waaminifu na wenye kufanya kazi kwa uzalendo. 

Waziri wa Nishati Dkt. Kalemani (katikati) akizungumza na wakazi wa kijiji cha Gumali, wilayani Maswa alipofika kukagua mradi wa REA III.

Waziri wa Nishati Dkt. Kalemani (katikati), mbunge wa Maswa Magharibi, Mashimba Ndaki( kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Maswa( kulia) Dkt. Seif Shekalaghe wakikagua orodha ya vijiji vitakavyopitiwa na Mradi wa REA III katika mzunguko wa kwanza wa REA IIII.


 
Waziri wa Nishati Dkt. Medard  Kalemani (kulia), na Kaimu Kamishna wa Nishati na Maendeleo ya Petroli,  Mhandisi Innocent Luoga wakikagua Miundombinu ya umeme iliyoanguka kutokana na upepo mkali uliombatana na mvua wilayani Maswa na kusababisha baadhi ya vijiji kukosa huduma ya umeme kwa siku kadhaa.


Kikundi cha ngoma ya asili kikitumbuiza kufurahia huduma ya umeme kufika katika kijiji cha Gumali wilayani Maswa, mkoani Simiyu.