Monday 5 March 2018

Marufuku kuvamia maeneo litakapopita Bomba la Mafuta - Lukuvi


Na Zuena Msuya, Kahama Shinyanga.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Wiliam Lukuvi amewapiga marufuku wananchi wenye tabia ya kuvamia maeneo yanayopitiwa na miradi mikubwa ya maendeleo kwa Lengo la kulipwa fidia ikiwemo Mradi wa ujenzi wa Bomba la kusafirisha mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga nchini Tanzania.

Lukuvi aliyasema hayo wakati akizungumza katika Warsha ya Wadau wa Bomba la kusafirisha Mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda Hadi katika bandari ya Tanga nchini uliofanyika wilayani Kahama,mkoani Shinyanga kwa Lengo la kutoa elimu juu ya mradi wa Bomba Hilo.

Alifafanua kuwa baadhi ya wananchi wamekuwa na tabia ya kuvamia maeneo yanayopitiwa na miradi mikubwa na kuyaendeleza kwa kupanda miti na kujenga nyumba ili waweze kulipwa fidia, Jambo ambalo halikubaliki.

Aliweka wazi kuwa mpaka sasa tayari wameshapiga Picha za awali katika maeneo yote yatakayopitiwa na mradi huo ili kurahisisha zoezi la ulipaji fidia kwa wananchi watakaoposha mradi huo.

“Kuna baadhi ya wananchi wakiona mradi mkubwa unapita wanaanza kuweka nguvu kubwa ya kujenga nyumba ambazo haziishi watu ili mradi tu wategeshe, mwingine anahamisha miti ya minazi au mkorosho ili afidiwe, hii si sawa! wananchi acheni tabia hiyo, na kila mmoja awe mlinzi kwa mwenzake na tuelezane ukweli kuhusu Miradi ya Maendeleo kwa faida yetu sote," Alisema Lukuvi

Akizungumzia zoezi la ulipaji fidia, Lukuvi alisema Serikali haitamuonea mtu yeyote na kila mmoja atalipwa kile anachostahili kulipwa kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi.

Aidha aliwataka Maafisa Ardhi kwa kushirikiana na Viongozi wa Serikali za Mitaa pamoja na vijiji kutoa elimu sahihi juu ya ulipaji wa fidia kwa wananchi kwa mujibu wa Sheria ya ardhi ili kuepusha changamoto zitakazoweka kujitokeza hapo baadaye.

Lukuvi aliweka wazi kuwa katika zoezi la ulipaji wa fidia kwa wananchi viwango vitakavyotumika ni vile vilivyopo katika Sheria ya Ardhi ya Tanzania hivyo wananchi waridhike na kile watakacholipwa kwa wakati huo.
Aidha aliwataka wananchi kutokwamisha ujenzi wa mradi huo kwa namna moja ama nyingine pia amewasihi kushirikiana na wale watakaokuwa wakifanya kazi katika maeno husika ili kurahisisha ukamilishwaji wa ujenzi wa Bomba hilo kwa haraka zaidi kwa kuwa mradi huo una manufaa kwao na taifa kwa ujumla.

"Endapo mtu amejenga eneo la hifadhi ambapo Bomba hilo litapita hatalipwa fidia, kwa kuwa fidia itatolewa kwa wale tu ambao maeneo ya yemepitiwa na Bomba hilo na si wale waliovamia maeneo ya hifadhi ya barabara kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi," alifafanua Lukuvi.

Mradi wa Ujenzi wa Bomba la kusafirisha mafuta ghafi unahusisha Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali ili kufanikisha ujenzi wake ikiwemo Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Wizara ya Fedha na Uchumi, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano pamoja na Wizara ya Mambo Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.


Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wiliam Lukuvi (kulia) akiwasili katika Warsha ya Bomba la kusafirisha Mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda Hadi katika bandari ya Tanga nchini iliyofanyika wilayani Kahama, mkoani Shinyanga kwa Lengo la kutoa elimu juu ya mradi wa Bomba Hilo.


Baadhi ya wadau wa Warsha ya Bomba la kusafirisha Mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi katika bandari ya Tanga nchini iliyofanyika wilayani Kahama, mkoani Shinyanga kwa Lengo la kutoa elimu juu ya mradi wa Bomba hilo.



Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wiliam Lukuvi (katikati), Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (kushoto) na Naibu Waziri wa Nishati Subira Mgalu(kulia) wakati wa Warsha ya Wadau wa Bomba la kusafirisha Mafuta ghafi kutoka Hoima  nchini Uganda Hadi katika bandari ya Tanga nchini iliyofanyika wilayani Kahama mkoani Shinyanga.
 

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wiliam Lukuvi, akizungumza wakati wa Warsha ya Wadau wa Bomba la kusafirisha Mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda Hadi katika bandari ya Tanga nchini iliyofanyika wilayani Kahama mkoani Shinyanga kwa Lengo la kutoa elimu juu ya mradi wa Bomba Hilo.